Chat Now

HABARI MPYA

FUNDISHO LA MSINGI

PICHA NA MATUKIO

CAPACITY BUILDING CLASS

MAHUSIANO

NUKUU YA LEO

IKIWA LEO NI SIKU YA WANAWAKE DUNIANI; MWANAMKE HUYU ASEMA: ''NATEMBEA NA BARUA YA KIFO MKONONI''



Veronica Kibuga (katikati) pamoja na watoto wake.  

HABARI KAMILI: 
Hebu fikiri... Unaamka asubuhi na kukuta kundi la majirani nje ya mlango wa nyumba yako. Uwepo wao siyo kwa lengo la kukusalimu, bali kukupa ujumbe wa hatima ya maisha yako.
Hali hii ndiyo iliyomkuta Veronica Kibuga (85) mkazi wa Kitongoji cha Kahangala wilayani Magu, Mwanza ambaye kwa miezi kadhaa amekuwa akiishi kwa hofu kwani anasubiri utekelezaji wa ‘adhabu ya kifo’ kukatwa kwa mapanga kutokana na tuhuma kuwa yeye ni mchawi.
Ujumbe uliotumwa kwake uliandikwa kwa lugha ya Kisukuma na ulikutwa kisimani ambako waliupeleka walipokwenda kuteka maji na unasema: “Bamayo yashikaga izamu igawo ya kukatwa mapanga”, ukimaanisha: ‘Imefika zamu yako ya kukatwa mapanga’.
Majirani wamejaa nje ya nyumba ya Kibuga kwani wanafahamu fika kwamba mwandishi wa ujumbe ule hatanii, kwani wote waliowahi kupata ujumbe kama wake waliuawa. Huyu ni mmoja, lakini ukweli ni kwamba wanawake wengi, hasa wazee wanaishi na makovu na wengine wamepoteza maisha baada ya kupokea taarifa kama hizi.
Wakati dunia nzima ikisherekea Siku ya Mwanamke Duniani leo hii, wanawake wa aina ya Kibuga wako ndani wamejifungia wakihofu usalama wao kutokana na kuishi katika jamii ambayo inamwona kama mkosi na chanzo cha matatizo yote.
Wanawake wanasherehekea leo na kutukuzwa kwa mchango wao mkubwa katika masuala mbalimbali, lakini wapo wanaohitaji ukombozi ili watoke kwenye madhila ambayo yamewafanya kuishi kwa wasiwasi mkubwa.
Hata watoto wadogo wanapofariki, huwa inaaminika kuwa mwanamke mchawi ndiye ‘aliyemla nyama’. Dhana hii imewafanya baadhi ya wanaume vijijini kuwaachia wanawake kazi ya kuchimba makaburi.
Haya ndiyo yaliyomkuta Kibuga ambaye leo hii anatembea na waraka wa kifo mkononi, akisubiri ‘siku ya hukumu yake’.
Simulizi yake
Kabugu anasema: “Siku moja niliamka asubuhi na kukuta majirani zangu wakiwa nje ya nyumba yangu, walikuwa wameniletea ujumbe wa kifo kutoka kwa mtu asiyejulikana akisema ataniua mimi na watoto wangu kwa kuwa ni wachawi.”
Barua hiyo iliyotumwa na mtu anayejiita ‘Meneja wa Kujiajiri’ ilieleza kuwa Januari 30 atafika katika nyumba ya bibi huyo na kummaliza kwa kumkata mapanga yeye na familia yake.
Watoto wa Veronica ambao ni Usia na Magdalena Kibuga nao wametajwa kuwa watauawa pamoja na mama yao kwa kuwa wanasaidiana naye katika masuala ya uchawi.

“Nimekuwa na hofu ingawa tarehe yenyewe imeshapita. Ninaogopa kwa sababu wenzangu wengi wamewahi kupata barua kama hizi na kupigwa kwa mapanga mpaka kufa,” alisema Kabuga.
Akizungumzia ulipoanzia mkasa huo anasema analihusisha tukio hilo na kugombea mashamba ambayo aliachiwa na marehemu kaka yake.
“Siku moja nilikuwa shambani nikilima ‘majaruba’ ya mpunga, alikuja mtoto wa marehemu kaka yangu na kuniambia niache kulima hapo kama sitafanya hivyo atanikatakata kwa mapanga. Ninahisi atakuwa ameamua kunizushia tuhuma za uchawi ili niuawe,” alisema Kabuga.
Alisema tishio hilo limemuathiri yeye na familia yake kwani wanashindwa kuendelea na shughuli za kilimo, wakihofu huenda mtu huyo anaweza kuwavamia shambani na kuwakata kwa mapanga.
“Tangu wakati ule imebidi tuishi katika nyumba moja, mimi pamoja na watoto na wajukuu zangu tunalala katika nyumba moja ili kujilinda. Hali hii imetufanya tushindwe kuendelea na shughuli zetu za kila siku,” alisema.
Watoto wake
Akizungumzia tukio hilo, Magdalena alisema wanaishi katika hali ya kukata tamaa kwani inavyoonekana Serikali imeshindwa kuwalinda, hivyo hatima yao ni kifo tu.
“Tumeamua kuishi pamoja na mama ili hao wauaji wakija watumalize tu, hatuwezi kufanya chochote na watu hawa inaonekana wameshindikana kabisa,” alisema Magdalena na kuongeza:
“Kwa miaka mingi haya matukio yamekuwepo, kama wenzetu wanauawa kila siku unafikiri sisi tutapona? Tunajua ipo siku watakuja tu kutukatakata lakini ukweli sisi siyo wachawi na wala hatuujui. Tunachoamini hawa wauaji wanakuwa na sababu nyingine tu.”
Uongozi wa Kitongoji
Mwenyekiti wa Kitongoji hicho, Mathias Ombesa alisema juhudi zinafanywa kuwalinda wanawake hao hata hivyo anakiri kuwa ni vigumu kutokana na mazingira halisi.
Ombesa alisema kutokana na wanawake hao kuishi katika nyumba ambazo milango yake ni ya kusukuma, hurahisisha kazi ya wahalifu katika kutekeleza maazimio yao.

“Kama unavyoona nyumba moja ipo hapa na nyingine iko kule mbali, siyo rahisi kuifikia hata unaposikia mtu akiomba msaada na utakapofika pale, utakuta mhalifu ameshatekeleza azma yake. Pia kama nyumba angalau ingekuwa na mlango imara ingesaidia kuwafanya hawa wahalifu wasiingie kwa urahisi,” alisema Ombesa.
Akizungumzia sababu za kushamiri kwa matukio kama hayo alisema kwamba mila na desturi bado zinamkandamiza mwanamke kwa kumhusisha na matukio ya uchawi baada ya kuzeeka.
“Hapa watu wengi wanaamini wazee wanawake ndiyo wachawi. Mfano mtu anapokuwa na mtoto wake mgonjwa, bibi kizee akimtajia dawa na akapona, moja kwa moja humuhusisha na uchawi na hoja yake huwa, kama ameweza kumponya mtoto basi anaweza kumroga,” alisema Ombesa.
Akizungumza mratibu wa Shirika la Maperece linalojishughulisha na kampeni ya kupunguza mauaji ya vikongwe wilayani Magu, Athanasio Kweyunga alisema umaskini ni chanzo cha mauaji hayo kwa kuwa hakuna tajiri ambaye huhisiwa kuwa mchawi.
“Umaskini unawaathiri wanawake, kwa mfano anapopikia kuni kwa muda mrefu macho yake huwa mekundu. Pia wajane huishi katika nyumba mbovu kutokana na kuwa na uwezo mdogo,” alisema Kweyunga.
Aliongeza kuwa kupungua kwa ardhi kutokana na ongezeko la watu ni sababu nyingine inayoongeza mauaji hayo, huku akisema kuwa wanachofanya ni kuwaelimisha vijana namna ya kuitumia ardhi ndogo wanayorithi kutoka kwa wazazi wao.
“Uchunguzi tuliofanya, tumegundua kuwa mauaji mengi yamekuwa yakifanywa na wanafamilia na chanzo huwa ni kugombea ardhi au mifugo. Vijana wanataka kumiliki sehemu kubwa ya ardhi na njia pekee ya kuipata ni kuwaua wazee,” anasema Kweyunga.
Alisema shirika hilo linawaelimisha vijana pia kuwawezesha wazee ili kuondokana na umaskini ambao huwafanya wahusishwe na imani za uchawi.
Chikawe anena
Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mathias Chikawe alisema Serikali italifuatilia suala hilo na kutoa ulinzi kwa watu waliopewa vitisho.
Aliongeza kuwa anawaomba wananchi hao watoe ushirikiano kwa askari ili kusaidia juhudi za Serikali katika kukomesha mauaji hayo.
“Kazi ya polisi ni kulinda raia na mali zao, nitasimamia kuona wanawake hao na wengine wanalindwa dhidi ya ukatili wa aina yoyote. Ninawaomba wananchi wasaidie katika kutoa taarifa ili watuhumiwa wafikishwe mbele ya sheria,” alisema Chikawe.

Source:
Mwananchi.



Juu