Chat Now

HABARI MPYA

FUNDISHO LA MSINGI

PICHA NA MATUKIO

CAPACITY BUILDING CLASS

MAHUSIANO

NUKUU YA LEO

JITAMBUE SAIKOLOJIA: DALILI ZA KUMGUNDUA MPENZI ATAKAE KUJA KUWA MKOROFI NA MGOMVI MARA MKIANZA KUISHI PAMOJA


Yatupasa wote tuliopo katika mahusiano, kabla ya kuendelea na kufanya maamuzi fulani tuwe tunatazama pia dalili za hatari. Kwa upande mkubwa dalili hizi zimeegemea kuwasaidia zaidi jinsia ya kike kujua au kuwafahamu wanaume. Hii ni kwa sababu wanawake ndio ambao wamekuwa wakioyesha kuumizwa zaidi na kukatishwa tamaa na mabadiliko ya tabia za wanaume mara wanapozama katika dimbwi la mapenzi. Ingawa wapo pia wanaume wanaoumizwa kutokana na mabadiliko ya tabia za wapenzi wao, na wao pia waweze kuzitazama dalili hizi.

DALILI ZENYEWE HIZI HAPA:

1. Mpenzi wako anakuwa na wivu sana kwa ule muda unaotumia kuwa na wafanyakazi wenzako,

    marafiki na hata ndugu zako, ingawa sio kwamba anataka muda huo awe na wewe.

2. Anakuwa na tabia za kukuudhi na kukutawala, ataangalia sana kutoka na kuingia kwako, nyendo zako

    na hata matumizi yako ya fedha, na kama ukimuuliza kwanini anafanya hivyo atajitetea kuwa anakusaidia
    kufanya maamuzi sahihi.

3. Taratibu anakutenga na wote waliokaribu na wewe, pia anajaribu kukutenga na wale wanaoonekana
    kuwa msaada kwako kama vile wale unaowasiliana nao kwa simu, wafanyakazi wenzako na hata ndugu
    zako wa karibu.

4. Huwa na tabia ya kuwalaumu sana wengine kwa matatizo anayoyapata yeye. Mfano anapokosa kazi,

    anaposhindwa shuleni, anapokosa pesa nk. Kila kitu ni kosa la mtu mwingine na sio yeye.

5. Hukasirishwa na kuudhiwa na vitu vidogo vidogo na vya kawaida katika maisha ya kila siku, mfano

    akiambiwa afanye kazi zaidi ya muda wa ofisi, akiombwa amwangalie mtoto, anapopingwa katika kitu
    kidogo nk.

6. Anakuwa na tabia za kikatili kwa wanyama wafugwao “pets” na hata kwa watoto. Haumizwi pale

    anapoona maumivu au kuteseka kwa kiumbe kingine. Anaweza kujiona anacheza au anatania bila kujua
    anamuumiza mtoto au mnyama.

 7. Ni wenye tabia ya mabavu hususan katika tendo la ndoa, hawatojali hisia zako, umelala usingizini au
     unaumwa, bali hujali zaidi kuzitimiza haja zao.

8. Ni wenye maneno makali yakuumiza na ya kushusha hadhi, huweza kukuamsha usingizini ili akutukane au

    kukugombeza. Akianza malumbano hakupi upenyo wa kwenda kulala, anaweza kulalama usiku mzima.

9. Sio watu wakutabirika, ni watu wenye hisia za kubadilika badilika, mara muda huu anafuraha na

    kuonyesha mapenzi, mara ghafla kakasirika na kutaka kuadhibu mtu.

10. Anaweza akawa na historia ya tabia za kikorofi na kigomvi, labda amewahi kuwa na matukio ya

      kuwapiga marafiki zake, akijitetea kuwa alipitiwa tu na hasira.

11. Ni mwenye vitisho na tabia za kuashiria fujo, mfano kupenda kutishia akisema “nitakuzaba vibao”
      “nitakuuwa ‘I will kill you if….”, “nitakuvunja shingo”, “nitakufanyia kitu mbaya” n.k.

12. Mwenye tabia ya kupiga au kugonga vitu kwa hasira, kuvunja vitu vyako, kukurushia vitu wewe au

      watoto kwa hasira.

13. Hutumia nguvu anaposisitiza hoja yake, mfano, kukushika nguo au kukukandamiza ukutani na mara

      nyingine kukusukuma.

• Tafiti zimegundua kwamba, kama mtu anaonyesha tabia za fujo na kijeuri wakati wa urafiki au uchumba    kuna uwezekano mkubwa wa kuwa mtu wa hatari zaidi mara atakapoingia kwenye ndoa. Kamwe usijidanganye na kujifariji kwamba hivyo vijitabia anavyovionyesha sasa eti atabadilika tu mara mkioana. Sahau.

Kumbuka; fujo huzaa fujo, na ujeuri huzaa ugomvi na kwa haraka vyote hivi huua mapenzi kwa wale wanaopendana.


CHRIS MAUKI - Mtaalamu wa Saikolojia Ya Jamii na Ushauri. 

 KUMBUKA:
Kama Blog hii imekuwa ya baraka kwako, unaweza kui-support kwa kununua bidhaa yetu ya Mafuta Halisi Ya Alizeti ili kuendelea kukuletea mafundisho zaidi kutoka kwa watu mbalimbali waliofanikiwa.
Bei zetu ni nzuri na mafuta haya yanapatikana kwa bei za Jumla na Rejareja!

Wasiliana nasi kwa:
0659 700 002.  Asanteni na Mungu awabariki wadau wangu!



AL-QAEDA YAHUSISHWA NA SHAMBULIO LA WESTGATE SHOPPING MALL


 
SHAMBULIO la kigaidi lililofanywa nchini Kenya Jumamosi iliyopita na watu waliodhaniwa kuwa wafuasi wa Al- Shabab, sasa limeelezwa kutekelezwa na mtandao mpana zaidi wa kigaidi wa kundi la Al-Qaeda.


Baadhi ya wachambuzi na wachunguzi wa masuala ya kiusalama na kimataifa, wameyataja mambo matatu ambayo yanathibitisha pasipo shaka kwamba waliotekeleza tukio hilo la kuvamia, kuteka nyara na kuua watu wapatao 68 katika Kituo cha Biashara cha Westgate, ni wa aina ya kundi ambalo kinadharia na kimatendo linafanana na lile la kigaidi duniani la Al-Qaeda. Mambo yanayotajwa na wachambuzi na wachunguzi hao ni pamoja na mbinu, teknolojia na aina ya watu waliotumika kutekeleza shambulio hilo.

Katika uchambuzi wao, wameeleza kuwa mbinu iliyotumiwa na magaidi hayo kuvamia pasipo kujulikana mara moja na vyombo vya ulinzi na usalama vya nchini Kenya, lakini pia aina ya silaha walizokuwa nazo, inaonyesha kuwa kundi hilo limeamua kutumia kivuli cha Al-Shabab kufikisha ujumbe kwa dunia kwamba lipo licha ya uongozi wake kubadilika.

Kwamba mbali na mbinu pamoja na teknolojia, pia aina ya watu waliohusika kutekeleza shambulio hilo ambao wamebainika kutoka katika mataifa mbalimbali duniani, ndio ambao wamewafanya wachambuzi na wachunguzi hao waanze kupata shaka kwamba huenda kuna kundi kubwa zaidi lililotekeleza shambulio hilo, ambalo limejivika taswira ya Al-Shabab.

Watu wanaotajwa kuvamia kituo hicho cha biashara na kutekeleza unyama wa kutisha, wanaelezwa kutoka katika mataifa ya Somalia, Uingereza, Marekani na Syria.

Taarifa hizi zinathibitishwa na kauli iliyotolewa juzi na Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Amina Mohamed ambaye katika mahojiano yake na Kituo cha Televisheni cha Al-Jazeera, alisema kuwa Al-Shabab hawakuwa peke yao katika shambulio hilo.

Mohamed aliiambia Al - Jazeera kuwa al-Qaeda ndio waliokuwa nyuma ya tukio hilo na si Al-Shabab.

“Al-Shabab hawafanyi peke yao, hili shambulio ni sehemu ya kampeni ya ugaidi wa kimataifa,” alisema Mohamed.
Waziri huyo alisema zaidi ya magaidi 20 wakiwemo wanawake, walikuwa nyuma ya shambulio hilo na kwamba watu hao wametoka katika mataifa tofauti tofauti duniani.

“Al-Shabab wanataka kujionyesha kwenye ngazi ya kimataifa, hasa baada ya kubadili uongozi na wanataka kuionyesha dunia kwamba wana nguvu bado, hivyo kuwekwa kwenye kundi la kulifikiria,” alisema.

Katika mahojiano yake mengine na kituo cha cha PBS cha nchini Marekani, Waziri Mohamed alisema washambuliaji kama wawili au watatu wamebainika kuwa ni raia wa Marekani na Mwingereza mmoja.

Ni kutokana na taarifa hizo, baadhi ya wachambuzi wanasema kuwa shambulio hilo la kigaidi lina ajenda zaidi ya Kenya.
Zipo hisia kwamba shambulio hilo halikuwa na lengo la kuiumiza Kenya pekee, kutokana na hatua yake ya kupeleka majeshi yake kwenda kupambana na kundi la kigaidi la Al-Shabab nchini Somalia, bali pia kumuumiza Rais wa Marekani, Barack Obama, ambaye kwa asili anatoka nchini humo.

Obama ambaye nchi yake imekuwa ikiongoza mapambano dhidi ya makundi ya kigaidi ikiwamo lile la Al-Qaeda, ambapo hivi karibuni ilifanikiwa kumuua kiongozi wake, Osama bin Laden, baba yake ni raia wa Kenya.

Baadhi ya wachambuzi wanasema kuwa, kitendo cha magaidi kuamua kukishambulia kituo hicho cha biashara cha Westgate, kinatokana pia na ukweli kuwa watu wengi wanaopenda kutembelea hapo ni raia kutoka mataifa ya Magharibi wakiwemo Wamarekani, hivyo ulikuwa ni mkakati wa kumuumiza Obama kwa njia hiyo.

Katika hotuba yake aliyoitoa siku ya Jumatatu, Rais wa Somalia, Hassan Sheikh Mohamud, alilielezea kundi la Al-Shabab kuwa ni tishio jipya kwa dunia.



Source: Fahamutz



NAWASHUKURU WASOMAJI WANGU, SASA TUMEFIKIA WASOMAJI ZAIDI YA ELFU ISHIRINI NA NNE 24,000. ENDELEA KUWASHIRIKISHA NA WENGINE.

JITAMBUE SAIKOLOJIA: JE MPENZI WAKO NI MWENYE HASIRA?

 

TAMBUA NINI CHA KUFANYA!

 
  By Chris Mauki, Mtaalamu wa saikolojia na jamii/mahusiano.

   Katika mahusiano ya aina yeyote hakuna  anayeweza kusema  hajawahi kukasirika.  Mara kwa mara tunakwazana na kukasirishana ingawa wako wale ambao hasira yao ipo karibu zaidi na huja  kwa ukali zaidi na mara nyingine huleta madhara katika vitu, watu, au hisia za mpenzi mwingine. 

Hapa nataka nikusaidie jinsi ambavyo unaweza kufanya pale mpenzi wako anapowaka hasira kali.  Kujua hili kutakusaidia kupooza  au kuponya hasira za mwenzako na sio kuchochea moto mkubwa zaidi ambao unaweza kuleta madhara makubwa zaidi. 

NINI CHA KUFANYA!
  1. Ikubali hasira ya mwenzako kama ndio njia yake ya kuonyesha hisia zake.
Hasira yake na kulipuka kwake kunaweza kuja kwa style ya kuleta  maudhi sana na  wala kusikokuwa na sababu ya msingi, lakini kubali kuwa ana haki ya  kuwa na hasira.  Hasira yake yaweza isiwe nzuri kwako lakini kumbuka haiashirii mwisho wa mahusiano yenu. Mahusiano yaliyo bora huruhusu kwa kiasi fulani vimikikimikiki kama hivi, huwezi kupinga visiwepo kwa asilimia 100.
 
  1. Mfanye mpenzi wako kuwajibika kwa hasira yake mwenyewe
Najua anaweza kukulaumu wewe kwa hasira zake, iwapo hali hii inatokea kataa kukubali wazo hilo, wewe hauhusiki kwa chochote, wala wewe sio sababu ya  hasira hizo bila  kujali  yeye anasema nini. Yeye ndio amechagua kukasirika na kufanya hivyo anavyofanya, na mara nyingi ni mbinu yake ya kukufanya ukubaliane na matakwa yake.  Kwa hali yoyote kataa kuchezewa kupitia hasira yake.
 
  1. Tulia na uwe na sababu ya kutulia kwako
Hata kama mpenzi wako kavuka mipaka kwa kukutukana, kukulaani, kukupayukia au hata kukupiga, bado waweza kuchagua kuwa mpole na mwenye sababu maalum ya kutulia kwako.  Taratibu na kwa upole mtulize kwa kumwonyesha uhalisia wa tukio.  Kwa busara na kujizuia kwa hali ya juu, jitahidi kumweleza mawazo yako, hisia zako na ukionyesha jinsi hali hiyo inavyokusumbua mara inapotokea, kamwe usitumie sentensi za “wewe” mfano “wewe unaudhi sana”, “Wewe sikuelewi kabisa” bali tumia sentensi za  “mimi”, mfano “mimi ninaumia sana unapofikia hali hii”.  Endelea kutoa mawazo yako kwa ufasaha na katika hali ya kumjali.
 
  1. Weka mipaka kwa hasira zisizo na sababu ya msingi
Kama mwenzako anazidi kuonyesha hasira yake isiyo na msingi, anatukana na kuendelea kubwatuka tu, na wala hakusikilizi unachotaka kukisema, basi unaweza kuamua kutoka  na kuwa pembeni ya eneo hilo, kwa upole mwambie kuwa utafurahi kuzungumzia  jambo hilo  mara atakapopoa ukali na  baada ya hapo nenda chumba kingine mpaka atulie.
  1. Jizuie usiombe msamaha au kumtaka radhi
Najua watu wengi, hususan jinsia ya kike wakifikia hatua hii hujiona wao ndio wakosaji na hivyo kukimbilia kuomba radhi.  Kumbuka kuwa mpenzi mkorofi na mtukanaji hastahili kuombwa radhi.  Ni kweli yawezekana  wewe ni sababu kwa kiasi fulani kwa tatizo hilo lakini kwa kule kukasirika kwa style hiyo hakumfanyi astahili kuombwa radhi maana kwa kufanya hivyo utaendeleza tabia yake hiyo mbaya.  Msamaha au radhi yaweza ikafaa baadae kidogo wakati mpenzi wako ametulia na ameiweza hasira yake. Jaribu kuihifadhi samahani yako mpaka wakati huo ufike.
 
  1. Mpongeze mpenzi wako mara tu anapoamua kufanya lile lenye staha na wala siyo anapoonyesha hasira.
Wakati wowote mpenzi wako anapoonyesha kushuka na kuelewakuwa analofanya sio jema, mpongeze, mtie moyo aendelee na tabia hiyo njema kwa kumwonyesha utayari wa kumsikiliza kile anachotaka kusema ili mfikie maafikiano. Katika mahusiano jifunzeni kuzipongeza na kuzitia moyo tabia na matendo mema na pia kuyazuia yale yasiyomema yasiendelee.
 
  1. Jipongeze Pia
Kamwe usiruhusu matukano, kejeli na kashfa za mpenzi wako zikuvunje moyo na kukushusha thamani yako.  Usijione mnyonge kwa lawama zake labda tu uchague kukubali anachokisema kwako.  Jione bado kuwa wewe ni mwema na ulikuwa unafanya mambo kwa nia njema.  Ukiweza jipongeze kwa kufanya kile ambacho hisia zako zitaona zimepongezwa.  Mfano, jitoe mtoko, nenda kwenye filamu, jipikie kitu kizuri, fanya nafsi yako ijisikie iko juu. Kama unajiona kuwa huwezi au unapata shida zaidi kuzifuata njia hizi basi jitahidi kumtafuta mshauri wa kisaikolojia “counselor” kwa msaada zaidi.
NAWASHUKURU WASOMAJI WANGU, SASA TUMEFIKIA WASOMAJI ZAIDI YA ELFU ISHIRINI NA NNE  24,000. ENDELEA KUTEMBELEA MARA KWA MARA NA KUWASHIRIKISHA WENGINE PIA.

TANGAZO LA UFADHILI KWA WASANII CHIPUKIZI WA FILAMU NA MUZIKI

1.     Wewe  ni  msanii  chipukizi  wa  filamu au  maigizo ?
2.     Wewe  ni  mwandishi  chipukizi  wa  filamu  ?
3.     Wewe  ni  mtayarishaji  chipukizi  wa  filamu ?
4.     Wewe  ni  muimbaji / mwanamuziki  chipukizi 
 Unataka  kukamilisha  ndoto  zako  lakini  haujui  pa  kuanzia ?  Kama  jibu  ni  ndio  basi  hii  ni  habari  njema  sana  kwako.
Taasisi  ya  RafikiElimu  Foundation  inapenda  kuwatangazia  wananchi  wote  kuwa  sasa,  tumeanza  kutoa  ufadhili  na  udhamini  kwa   wasanii  chipukizi  wa  filamu, waandishi  chipukizi  wa  filamu, watayarishaji ( Producers )  chipukizi  wa   filamu   pamoja  na  waimbaji(wanamuziki ) chipukizi   wenye  sifa  zifuatazo :
1.      Awe  na  kipaji  cha  kuigiza  AU
2.     Awe  na  kipaji  cha  uandishi  wa  filamu   AU
3.     Awe  na  nia  thabiti  ya  kuwa  mtayarishaji  wa  filamu  AU
4.     Awe  na  kipaji  cha  uimbaji.
5.     Awe  raia  wa  Tanzania  na  mkaazi  wa  jijini  Dar  Es  salaam.
6.     Awe  na  umri  wa  kuanzia  miaka  14   hadi   55.
     
     UTARATIBU   WA  KUTUMA  MAOMBI  
Tuma  maombi  yako  kupitia  barua  pepe  yetu  ambayo  ni  : rafikielimutanzania@gmail.com   . Maombi  yaelekezwe  kwa
Mkurugenzi  Mtendaji,RafikiElimu  Foundation, S.L.P  35967,
Dar  Es  salaam.
   AU 
Unaweza  kuleta  maombi  yako  moja  kwa  moja  katika  ofisi  zetu. Ofisi  zetu  zipo  katika  eneo  la  CHANGANYIKENI  karibu  na  CHUO  CHA  TAKWIMU. 
Kufika  katika  ofisi zetu,  panda  daladala  za  UBUNGO- CHANGANYIKENI  kisha  shuka  kituo  cha  TAKWIMU  halafu  tembea  hatua  ishirini  mbele  kisha  tazama  upande  wako  wa  kulia  utaona  ofisi  imeandikwa  RAFIKIELIMU  FOUNDATION.
Mwisho  wa  kupokea  maombi  ni  tarehe  30  SEPTEMBA  2013.
Kwa  maelezo  zaidi   wasiliana  nasi  kwa  simu  0782405936  au  0756606085   

NAWASHUKURU WASOMAJI WANGU, SASA TUMEFIKIA WASOMAJI ZAIDI YA ELFU ISHIRINI 20,000. ENDELEA KUWASHIRIKISHA NA WENGINE.


Juu